Advertise with Us

Advertise with Us

DHall

DHall

Pages

November 1, 2013

Nchi inayoongozwa na kuendeshwa kwa Matukio aka "Division Five"

Tukiacha matukio mengi yaliyotukia na kupita ni kwamba kwa takribani miezi mitatu vyombo mbalimbali vya habari vimekuwa vikiripoti habari mbalimbali katika namna ambayo kwa mtu ambaye unafikiri kwa kina na kuona mbali unaweza kugundua jambo fulani kwamba inawezekana yote yanayotukia ni mambo ambayo tayari yamepangwa na hata kutukia kwake ni kwa kufuata series ambayo pale habari fulani inapokomea na kuanza kupotea katika masikio ya wengi ndipo hapo na habari nyingine inapoibuka, Tukianzia na habari ya Rasimu ya mabadiliko ya Katiba sambamba na Muungano wa vyama kadhaa vya kasiasa kushinikiza rais Jakaya Kikwete kutotia saini Muswada wa Marekebisho ya Sheria ya Mabadiliko ya Katiba na baadae rais Jakaya Kikwete kutoa hotuba ambayo sambamba na mambo mengine pia ilitoa maelekezo kuhusiana na kile vyama pinzani vilichokitaka.

Ilihali habari hiyo ikiwa haijapoa ikatoweka au kutoweshwa ghafla katika masikio ya wengi baada ya kamati ya Bunge ya kusimamia hesabu za mashirika ya umma (PAC) kupitia mwenyekiti wake Zitto Kabwe kuvituhumu baadhi ya vyama vya siasa kwamba kwa takribani miaka minne havijafanyiwa ukaguzi wa hesabu za matumizi ya Ruzuku zinayoipata kutoka Serikalini habari ambayo ilivuma sana kutokana na baadhi ya vyama vingi vya siasa kujibu mapigo ya mwenyekiti huyo wa PAC hususani CHADEMA ambacho kilijitetea vyema na kuthibitisha kwamba tuhuma hizo zilikuwa sio za kweli bali zililenga katika kukichafua kinyume kabisa na sheria zinazohusiana na vyama vya siasa zinavyoelekeza kibaya zaidi ni ikiwa Mwenyekiti wa kamati hiyo Zitto Kabwe kuwa ni Naibu Katibu Mkuu wa CHADEMA habari hiyo iliongelewa sana hata wengine kusema kwamba lengo la Zitto Kabwe lilikilenga chama chake zaidi na wala sio vyama vingine kama wengi walivyokuwa wakidhani, Haikuishia hapo bali ikaibuka habari ya Mwenyekiti wa Kamati ya kusimamia hesabu za mashirika ya Umma (PAC) Zitto kabwe kwenda nchini Uswisi na nchi nyinginezo za bara la ulaya kufuatilia taarifa za Vigogo mbalimbali ambao wanadaiwa kuficha mamilioni yao (Fedha halali na zisizo halali) katika nchi hizo. Habari hiyo ilipokelewa juu kwa juu na kabla hata haijaanza kuvuma muendelezo wa kile wachunguzi wa mambo walichokidai kwamba ni kushindwa kwa mbinu ya kukichafua Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kupitia madai ya kutokaguliwa kwa hesabu za matumizi ya ruzuku ya chama hicho kwa miaka minne na muendelezo huo ukaonekana kuunganishwa kwa kitendo cha aliyekuwa Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo CHADEMA Mkoa wa Arusha Samsoni Mwigamba kukiuka Katiba, Kanuni na Taratibu za chama na kutumia jina bandia mtandaoni kuibua tuhuma nzito akikituhumu chama chake haswa uongozi wa juu wa chama hicho (Katibu na Mwenyekiti) kujihusisha na vitendo vya hila ili kuendelea kuwa viongozi wa chama hicho kinyume na katiba na sera za chama hicho huku akitumia sehemu kubwa ya waraka wake kumsifia Naibu Katibu Mkuu wa chama hicho Zitto kabwe karibu katika kila aya ya waraka huo jambo ambalo lilizua migongano na majibishano mitandaoni baina ya wanachama, wapenzi na mashabiki mbalimbali wa CHADEMA hata wale ambao wako kinyume au tofauti na chama hicho hususani CCM ambao daima furaha yao ni kuona CHADEMA inagubikwa na mitafaruku, migongano na makundi ambayo nia kubwa ni kukivuruga chama hicho ambacho kimekuwa tishio hata kwa Chama Cha Mapinduzi (CCM) baada ya kuonekana wazi kwamba kwa namna mienendo ya viongozi wake ilivyo kuna uwezekano kwa chama hicho kuchukua dola katika uchaguzi wa mwaka 2015 kama ambavyo ilithibitishwa na Mwenyekiti wa CCM Taifa, Rais Jakaya Kikwete ambaye kutokana na vitendo mbalimbali viovu na vichafu vinavyofanyika ndani ya chama chake alisema "kama rushwa haitakomeshwa ndani ya chama hicho, katika uchaguzi mkuu utakaofanyika mwaka 2015 kitaanguka vibaya na iwapo kitanusurika hakitapita kwenye uchaguzi mkuu wa mwaka 2020.

Katika hatua nyingine, Rais Kikwete amempa jukumu la kushughulikia viongozi wa CCM wanaokula rushwa, Makamu Mwenyekiti wa CCM, Philipo Mangula.Rais Kikwete, alitoa onyo hilo juzi usiku, alipokuwa akifunga mafunzo maalumu ya siku nne kwa makatibu wa mikoa, makatibu na wenyeviti wa wilaya wa chama hicho nchini.“Kama hatutabadilika katika suala la rushwa mwaka 2015 tutakuwa na wakati mgumu sana na kama mwaka huo tutafanikiwa kuishika Serikali, basi mwaka 2020 hatutarudi tena madarakani. “Najua rushwa ipo na mnaendelea kupokea shilingi laki mbili za airtime (muda wa mawasiliano), ndugu zangu hatutafika ama wengine watavuka na wengine kukwama,” alisema Mwenyekiti wa CCM, Rais Kikwete. Hii ni kauli ya kwanza nzito ya Rais Kikwete ya hivi karibuni ya kukionya chama hicho kuhusu uimara wake wa kuendelea kushika dola.“Viongozi wa chama ndio mmekuwa mawakala wa kusambaza rushwa bila hata aibu. Nawaombeni tubadilike, kama tutaendelea hivi hali yetu itakuwa ngumu sana katika chaguzi mbalimbali, nawaambieni,” alisema Rais Kikwete ambaye alitumia muda wa saa mbili kufunga mafunzo hayo. Aliwaambia kuwa siku hizi watu wana mbadala wa vyama vingine na siyo CCM peke yao.. Aliendelea kusema kuwa tatizo la rushwa kwa viongozi wa chama hicho linazidi kuwa kubwa kila siku, hali ambayo inawapotezea imani wananchi ambao ndio wapiga kura wao.

Ilihali hiyo yote ikiendelea Serikali imebadilisha viwango vya ufaulu wa elimu ya kidato cha nne na sita ambapo daraja la sifuri sasa limefutwa na imeongeza daraja la tano kiwango cha alama ya F ambayo sasa itakuwa alama kati ya 0 hadi 20. Hayo yamesemwa na katibu mkuu wa wizara ya elimu na mafunzo ya ufundi Profesa Sifuni Mchome wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusu mabadililo hayo.Mpaka hapo unaweza kupata picha japo kidogo ni kwa namna gani mambo yanavyoendeshwa au kupelekwa kwa namna ambayo haikupi nafasi wewe kama mwananchi kupata kufahamu mrejesho au muafaka wa kila jambo (Habari) kwa manufaa yako na taifa kwa ujumla kama inavyotakikana na badala yake taarifa au habari nyingi zikionekana kuwa ni za kuibua mambo na kuyaacha hewani badala ya kuyachunguza, kuyaibua, kuyafuatilia na kuyapatia mrejesho na hatimaye suluhisho kwa faida ya wananchi na taifa zima kwa ujumla .

No comments:

Post a Comment